Kwa mujibu wa taarifa, katika mkutano wao, viongozi hao wawili walisisitiza umuhimu wa kustawisha maelewano ya kidini duniani.
Papa Francis pia ametoa wito wa kuimarishwa ushirikiano wa Vatican na Al Azhar katika kustawisha utamaduni wa wafuasi wa dini mbali mbali kuishi pamoja kwa amani.
Aidha amesema asasi kubwa za kidini zina nafasi muhimu katika kustawisha thamani kama vile amani na watu kurehemeana na kuhurumiana. Kwa upande wake, Sheikh Tayeb alisema mkutano wake na Papa Francis ni sisitizo la maelewano ya kidini.
Papa Francis na Sheikh Tayeb walitia saini Waraka wa Maelewano ya Binadamu kwa ajili ya Amani Duniani na Kuishi Pamoja katika Kongamano la Kimataifa la Kidini lililofanyika mjini Abu Dhabi katika Umoja wa Falme za Kiarabu mwezi Februari.