Rais Ebrahim Raisi ameyasema leo mjini Tehran alipohutubu kwa mnasaba wa Siku ya Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Akihutubu katika gwaride hilo ambalo limeandaliwa katika Haram ya Imam Khomeini MA kusini mwa Tehran, Rais Raisi amesema, Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yana uwezo mkubwa sana. Amesema msingi wa uwezo huo ni wanajeshi wenye ikhlasi ambao wako tayari kuingia katika medani na kupambana na kila aina ya adui.
Rais Rais ameuonya vikali utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kusema: " Utawala wa Kizayuni unafahamu harakati yake ndogo zaidi inafuatiliwa kwa karibu na majeshi yetu. Wkifanya kosa lolote, majeshi yetu yatafika katika kitovu cha utawala wa Kizayuni ambapo uwezo wa majeshi yetu hautawaacha katika utulivu."
Ameendelea kusema kuwa Jeshi la Iran limebadilisha vikwazo kuwa fursa katika sekta ya viwanda vya kijeshi na kufanikiwa kupata uwezo mkubwa.
Halikadhalika amesema leo Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni jeshi ambalo lina zana za kutosha na liko tayari kuilinda nchi na mfumo wa Kiislamu. Ameongeza kuwa, kuwa tayari kivita Jeshi la Iran ni ujumbe wa matumaini kwa marafiki wa Mapinduzi ya Kiislamu nao maadui wafahamu kuwa uwezo wa majeshi ya Iran ni wa kujihami.
Rais Raisi amesema ujumbe wa uwezo wa majeshi ya Iran ni ujumbe wa nguvu kwa wote waliodhoofishwa, wanaodhulumiwa na wanaokandamizwa kwamba vikosi vya jeshi la Iran ndio ndio nukta yao ya matumaini.